Tarehe 9 Februari 2026, Ubalozi ulifanya mazungumzo na wawakilishi wa Kampuni ya ZENSHO, miongoni mwa makampuni makubwa ya chakula nchini Japan. Mazungumzo hayo yalilenga kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na Kampuni ya ZENSHO katika maeneo ya biashara, uwekezaji wa kijamii, kilimo, lishe, na maendeleo ya rasilimali watu.

Katika mazungumzo hayo, wawakilishi wa ZENSHO waliishukuru Tanzania, miongoni mwa nchi nyingine za Afrika, kwa kuunga mkono msimamo wa Japan wa kupinga pendekezo la kuweka vikwazo vya biashara ya kimataifa ya samaki aina ya eel. Pendekezo hilo lilijadiliwa na hatimaye kukataliwa katika Mkutano wa Kimataifa wa CITES COP20 (Convention on International Trade in Endangered Species of Wild Fauna and Flora) uliofanyika mwezi Novemba 2025 nchini Uzbekistan. Walieleza kuwa uamuzi huo ni muhimu kwa utamaduni wa chakula cha Japan pamoja na kwa shughuli za kibiashara za Kampuni ya ZENSHO.

Aidha, Kampuni ya ZENSHO ilieleza kuwa imeanza kutekeleza miradi ya kijamii barani Afrika, hususan kupitia Mradi wa Lishe Mashuleni. Kupitia mradi huo, wanafunzi wa shule za kilimo wanahusishwa na ufugaji wa kuku na uzalishaji wa mayai, ambayo husambazwa kwa shule za msingi zilizo jirani kama chakula cha mchana, kwa lengo la kuboresha lishe ya watoto kwa kuongeza ulaji wa protini ya wanyama.

ZENSHO ilifafanua kuwa mradi huo umeanza katika hatua ya majaribio (pilot phase) katika nchi jirani na Tanzania, ambapo kuku wapatao 400 wamehusishwa katika shule moja ya kilimo. Ilielezwa kuwa kuna mpango wa kupanua mradi huo ndani ya nchi hiyo na baadaye kuutekeleza katika nchi jirani, ikiwemo Tanzania. Kampuni ilionesha nia ya kufanya ziara nchini Tanzania kwa ajili ya majadiliano zaidi na mamlaka husika za elimu, na ikaomba ushirikiano wa Ubalozi katika kuratibu mawasiliano na maandalizi ya ziara hiyo, yatakapokamilika.

Vilevile, Kampuni ya ZENSHO ilieleza kuwa inaendesha Programu ya Mafunzo kwa Vitendo (Internship Program) kwa wanafunzi wa Kiafrika wanaosoma nchini Japan, kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Japan (JICA). Programu hiyo ni ya muda mfupi wa takribani wiki mbili, na huwapa wanafunzi fursa ya kujifunza mnyororo mzima wa thamani wa sekta ya chakula, ikiwemo uzalishaji wa kilimo, usindikaji wa chakula, usafirishaji, uhifadhi, na uendeshaji wa migahawa, pamoja na kujifunza masuala ya utamaduni wa Japan, ikiwemo sherehe ya chai ya Kijapani.

Ilielezwa kuwa mwaka 2025, wanafunzi watatu kutoka nchi mbili za Afrika Mashariki walishiriki katika programu hiyo, na kwamba mwaka 2026 Kampuni ya ZENSHO inapanga kupokea wanafunzi kati ya watano hadi sita kutoka nchi mbalimbali za Afrika, ikiwemo Tanzania. Kampuni iliomba Ubalozi kushirikiana nayo katika kuwatambua na kuwaunganisha wanafunzi wanaofaa kupitia vyama vya wanafunzi wa Tanzania nchini Japan, ikiwemo Tanzania Students Association in Japan (TSJ).

Kwa upande wa biashara, ZENSHO ilieleza kuwa kwa sasa inaagiza bidhaa za Tanzania kwa kiwango kidogo, hususan kahawa, na kwamba matumizi ya bidhaa nyingine kama ufuta, maharage, na chai bado ni madogo kwenye migahawa inayomilikiwa na Kampuni hiyo. Hata hivyo, Kampuni ilieleza kuwa ipo tayari kupokea sampuli za bidhaa za kilimo zilizochakatwa kutoka Tanzania, ikiwemo bidhaa zilizogandishwa au zilizokaushwa, kwa ajili ya tathmini ya uwezekano wa kuingia katika soko la Japan, ikizingatiwa vikwazo vilivyopo katika uingizaji wa mazao mabichi.

Ubalozi uliishukuru Kampuni ya ZENSHO kwa nia yake ya kuwekeza kijamii na kiuchumi barani Afrika, na ukaahidi kuendelea kushirikiana nayo katika kutafuta na kuendeleza fursa za ushirikiano zitakazonufaisha Tanzania, hususan katika sekta za kilimo, lishe, elimu, na maendeleo ya rasilimali watu.